Back to top

Korea kuisaidia Tanzania katika sekta za ujenzi,afya na nishati

22 July 2018
Share

Serikali   ya Tanzania na ile ya Jamhuri ya Korea zimekubaliana kushirikiana katika nyanja  mbalimbali zikiwemo zile za  afya na ujenzi lengo likiwa ni  kuwafanya wakazi wa nchi hizo mbili kuweza kunufaika na ushirikiano uliopo baina ya mataifa hayo mawili.

Waziri mkuu  Mhe.Kassim Majaliwa amesema hayo Jijini Dar es Salaam mara baada ya kumaliza mazungumzo yake na waziri mkuu wa Jamhuri ya Korea  Mhe. Mhe.Lee Nak-Yon na kuongeza kuwa baadhi ya matunda ya ziara hiyo ni Tanzania kunufaika na ujenzi mpya wa madaraja,barabara na hospitali  za kisasa.

Waziri mkuu na mgeni walishuhudia hafla ya  utiaji saini wa mkataba  wa mahusiano ya kidiplomasia ambayo yanahusu uondoaji wa visa za kusafiria  kwa wanadiplomasia na zile za utumishi yaliyofanywa na waziri wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa Dkt.Augustine Mahiga na makamu wa kwanza wa waziri wa mambo ya nje ya Jamhuri ya  Korea Lim Sung –Nam. 

Baadhi ya viongozi wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamesema ziara hiyo ni neema kwa Tanzania hasa katika taasisi wanazozisimamia kwani wanatumai mabadiliko chanya mengi yatakuwepo kutokana na mazungumzo yaliyofanyika.