Back to top

Rais Magufuli aguswa na Kifo cha King Majuto, atuma salamu za pole.

09 August 2018
Share

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ametuma salamu za rambirambi kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe kufuatia kifo cha msanii mkongwe hapa nchini Mzee Amri Athuman maarufu kwa jina la King Majuto kilichotokea tarehe 08 Agosti, 2018 Jijini Dar es Salaam.

King Majuto amefariki dunia majira ya saa 1:30 Jioni katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alikokuwa akipatiwa matibabu.

Katika salamu hizo Mhe. Rais Magufuli amemtaka Dkt. Mwakyembe kufikisha salamu zake za pole kwa familia ya Marehemu, Wasanii wote nchini, wadau wa sanaa, ndugu, jamaa, marafiki na wote walioguswa na kifo cha King Majuto.

Mhe. Rais Magufuli amesema King Majuto atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa na wa muda mrefu alioutoa kupitia sanaa ya uigizaji na uchekeshaji, ambapo alishiriki kuelimisha jamii, kuendeleza na kukuza sanaa na kuunga mkono juhudi za chama na Serikali katika kuhimiza maendeleo.

"King Majuto alikuwa kielelezo cha safari ndefu ya sanaa kwa nchi yetu, kwa muda wote amedhihirisha kipaji, ujuzi na uwezo wa hali ya juu katika uigizaji na uchekeshaji na hivyo kuwa kipenzi cha Watanzania na wasanii wenzake, hatutasahau ucheshi wake, upendo na uzalendo kwa nchi yake wakati wote wa uhai wake" amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli amesema anaungana na familia na wote walioguswa na kifo cha King Majuto katika kipindi hiki cha majonzi na amemuombea kwa Mwenyezi Mungu apumzike mahali pema peponi, Amina.

Inna lillahi wa inna ilaihi raji'un

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Dar es Salaam