Back to top

Rais Samia akutana na Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza Tony Blair.

22 July 2021
Share

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza Mhe. Tony Blair, Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Mhe.Tony Blair ambaye ni Mwenyekiti Mtendaji wa Taasisi ya Mabadiliko Ulimwenguni (Tony Blair Institute for Global Change) amemhakikishia Mhe. Rais Samia kuwa taasisi yake inaunga mkono jitahada mbalimbali anazochukua katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania.

Amesema taasisi yake inafanya kazi katika nchi 16 Afrika ikijikita kutekeleza vipaumbele vya Serikali zao ambapo amesema katika kipindi cha mwaka mmoja na nusu taasisi yake imejikita zaidi katika masuala ya kukabiliana na janga la UVIKO 19.

Mhe. Tony Blair amesema katika kukabiliana na janga la UVIKO 19, taasisi yake inashughulika zaidi na masuala ya upimaji na usambazaji wa chanjo ambapo amesema taasisi yake inaweza kusaidia Tanzania kuwafikia wazalishaji wa chanjo hizo.

Aidha, amesema mbali na masuala ya UVIKO 19, pia wanajengea uwezo nchi washirika kufuatilia miradi ya kilimo, nishati na matumizi ya teknolojia.

Kwa upande wake Mhe. Rais Samia amemshukuru Mhe. Tony Blair kwa kumjulisha masuala yanayofanywa na taasisi yake katika kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika nchi washirika.

Mhe. Rais Samia amesema kwa sasa Serikali inaendelea na uboreshaji wa mazingira bora ya uwekezaji kwa sekta binafsi ili kuwezesha utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP III) wa Tanzania.

Kuhusu UVIKO 19, Mhe. Rais Samia amemueleza Mhe.Tony Blair kuwa tayari Serikali ina mpango wake wa Kitaifa kuhusu namna ya kushughulikia masuala yote ya UVIKO 19 ikiwemo uratibu wa chanjo.