Mamlaka ya Mapato nchini TRA imesema mahusiano na ushirikiano kati ya mamlaka na wafanyabiashara umeendelea kuimarika na kuleta tija kwa wananchi na taifa kwa hatua ambayo mkurugenzi wa elimu ya mlipakodi Bw. Richard Kayombo amesema umeanza kurahisisha ulipaji wa Kodi na pia kupunguza gharama za ukusanyaji.
Akizungumza na walipakodi mkoani Arusha Bw. Kayombo amesema baada ya wafanyabishara kuanza kuelewa umuhimu wa kulipa kodi na pia kuona matokeo ya kodi zao asilimia kubwa sasa wanalipa kwa hiyari na wanatoa ushirikiano mkubwa ukiwemo wa kufichua wachache wanaoendelea kukwepa kodi na mbinu wanazotumia.
Kuhusu hatua iliyofikiwa kudhibiti ukwepaji wa kodi kwa bidhaa zinazotoka nje Bw. Kayombo amesema pia tatizo hilo linaendelea kupungua kutokana na kuimarishwa kwa ushirikiano na wenzao wa nchi jirani na ameendelea kuwaomba wafanyabishara kutumia fursa za soko la pamoja na Jumuiya ya Afrika Mashariki kufanya biashara halali ili kuepukana na hasara zisizo za lazima kwani biashara za magendo kwa sasa hazina nafasi.
Baadhi ya wafanyabishara wamekiri kuboreka kwa mahusiano miongoni mwao na TRA na wameitaka mamlaka hiyo kuendelea kuyaboresha hasa wakati huu ambao hali ni ngumu kwani hata wao wanafurahia kulipa kodi na wanaona matokeo yake.