Back to top

Zaidi ya watoto 3,000 wilayani Mwanga wapatiwa huduma za afya.

22 June 2018
Share

Watoto wanaoishi katika vijiji vilivyokumbwa na mafuriko katika wilaya ya Mwanga  mkoani Kilimanjaro wapo hatarini kukumbwa na magonjwa ya utapiamlo kutokana na ukosefu wa lishe bora.

Hayo yamebainishwa na daktari wa watoto kutoka Taasisi ya afya KCMC Dkt Jonstone George wakati wa zoezi la kutoa huduma za afya bure na vipimo vya magonjwa mbalimbali kwa watoto wadogo wenye umri chini ya miaka mitano kwenye vijiji  vitatu vilivyokumbwa na mafuriko katika wilaya ya Mwanga.

Katika zoezi hilo ambalo limeendeshwa na madaktari kutoka hospitali ya rufaa ya KCMC na wanafunzi wa Chuo kikuu cha tiba KCMC jumla ya watoto elfu tatu (3,000)wamepatiwa huduma za afya na wazazi kupewa elimu ya lishe kwa watoto hao ambao tayari wameabinika kuwa na viashairia na ugonjwa wa utapiamlo.

Akizungumza wakati wa kutoa huduma za afya kwa watoto katika zahanati ya Kifaru Mhadhiri wa Chuo kikuu cha tiba  KCMC Dk  Florida Muro amesema  lengo la kutoa huduma za vipimo kwa  watoto wa vijiji hivyo  ni pamoja na  kuhakikisha afya zao zinakuwa salama kwa kuwa  watoto ndiyo wanaoathirika zaidi wakati wa  majanga kama mafuriko yanapotokea.

Kwa upande wake Muuguzi Mfawidhi zahanati ya kifaru na baadhi ya wanawake wamesema  upatikanaji wa chakula kwa baadhi ya maeneo ni changamoto kubwa hali ambayo inasababisha watoto kukosa lishe bora.