Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Mtwara inatarajia kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wawili akiwemo mfanyakazi wa benki ya NMB wilaya ya Nanyumbu kwa makosa ya kugushi na utakatishaji wa fedha haramu kwa kuingiza jina la mtoto mwenye umri wa miaka 5 katika malipo ya korosho na kujipatia shilingi milioni tano kinyume na sheria za nchi.
Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Mtwara Stephen Mafipa amesema watuhumiwa hao ni Juma Mbevu ambaye ni Katibu wa mkuu wa NAPACHO AMCOS, na Agustino Nziku mfanyakazi wa benki ya NMB wilaya ya Nanyumbu, ambao wameshirikiana kufanya kosa hili.