Back to top

5 MBARONI KUJIFANYA MAOFISA TRA ARUSHA

23 November 2023
Share

Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha linawashikilia watuhumiwa watano kwa tuhuma za kujifanya maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kutapeli wananchi katika maeneo tofauti tofauti Mkoani humo.

Hayo yamebainishwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Justine Masejo, nakusema kuwa bado Jeshi hilo linaendelea kuwahoji watuhumiwa hao na pindi upelelezi utakapo kamilika jalada litapelekwa ofisi ya Taifa ya Mashtka kwa hatua zaidi za kisheria.

Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Justine Masejo amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Fredy Malaki (34) mkazi wa Karakata, Francis Mwita (42) mkazi wa Ukonga, Fidelis Joseph (27) mkazi wa Msumi Mbezi, Selina Fortunatus (43) makazi wa Temeke wote kutoka Jijini Dar es salaam na Fereji Hamadi (40) mkazi wa Tabora.

ACP Masejo ametoa wito kwa wananchi kujiridhisha na watu wanaofika maeneo yao ya biashara na kujitambulisha kuwa ni maafisa wa TRA ambapo amewaomba wananchi kutoa taarifa za baadhi ya watu hao wachache wanaofanya matukio ya uhalifu hususani ya utapeli katika Mkoa huo ili hatua za kisheria ziendelee kuchukuliwa dhidi yao.

Kwa upande wake Afisa wa kodi mwandamizi kutoka Mamlaka ya Mapato Bw. Hamenyimana Ayoub amesema mamlaka ya mapato imekuwa ikipokea malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusiana na uwepo wa baadhi ya watu wanaojiita maafisa wa mamlaka hiyo na kuchukua fedha.

Afisa huyo mwandamizi amendelea kufafanua kuwa baada ya kupokea taarifa hiyo alitoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ndipo kwa kushirikiana na Jeshi hilo pamoja na Wananchi walifanikiwa kuwakamata Watuhumiwa hao huko maeneo ya Manyara Kibaoni Wilayani Karatu wakati wakijaribu kutoroka.

Nae Bw Karatu John ambaye ni muhanga amebainisha kuwa watuhumiwa hao walifika dukani kwake na kujitambulisha kuwa ni maafisa wa mamalaka ya mapato (TRA) nakuanza kuwahoji huku wakitaka kulipwa kiasia cha fedha ya kitanzania Milioni nne na nusu.