Back to top

AGIZO LA RAIS SAMIA KUHUSU NGOs LATEKELEZWA

09 May 2022
Share

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum imetekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, alilolitoa jijini Dodoma Septemba 2021 kuhusu kuandaa mkakati kwa Mashirika yasiyo ya Kiserikali nchini wa kupunguza utegemezi katika utekelezaji wa majukumu yao.Hayo yamesemwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt Dorothy Gwajima wakati akifungua kikao cha wadau wa Mashirika yasiyo ya kiserikali kwa Kanda ya Mashariki kilicholenga kutoa maoni ya wadau hao katika kuweka mikakati ya kujisimamia na kupunguza utegemezi wa fedha za wafadhili.

Waziri Dkt.Gwajima alisema Mashirika yasiyo ya Kiserikali yamekuwa yakichagiza jitihada za Serikali kuwaletea Wananchi wake maendeleo kupitia utekelezaji wa miradi ya afua mbalimbali zikiwemo za Afya, Kilimo, Elimu, Maji, Mazingira, Miundombinu, Utawala Bora, Nishati, hifadhi wa Jamii, Mifugo na Uvuvi, Uwezeshaji wa Jamii na Sekta nyingine mtambuka. 

"Miradi hiyo, sio tu imewanufaisha Wananchi wetu kijamii, bali pia imechangia katika kuongeza ukuaji wa uchumi, kuboresha utoaji wa huduma na kuongeza fursa za ajira hususan kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu"Amesema Dkt.Gwajima

Ameongeza kuwa Wizara inashirikiana na wadau wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuandaa Mpango Mkakati wa kuyajengea uwezo Mashirika hayo ili kupunguza utegemezi na kuwa na uendelevu wa shughuli zao na utaratibu huo wa kukusanya maoni kutoka katika Mashirika hayo unafanyika katika Kanda tano ikiwemo Kanda ya Mashariki Kanda ya Kati, Kanda ya Magharibi, Kanda ya Kaskazini na Kanda ya Ziwa.

"Wizara ilianza mchakato kwa kuandaa Mkakati huo, tarehe 10 Novemba, 2021, ambapo iliunda Kamati ya wajumbe 20 ikijumuisha wataalam kutoka Wizarani, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, sekta binafsi na Wadau wengine."Amesisitiza Dkt Gwajima

Aidha Waziri Dkt.Gwajima alisema Kamati iliyoundwa mpaka sasa imefanikisha kukamilika kwa andiko la majadiliano (Consultation Paper), nyenzo za ukusanyaji wa taarifa na maoni kutoka kwa wadau mbalimbali (Stakeholders Engagement Tools), pamoja na ukusanyaji wa taarifa na maoni kutoka kwa wadau.

Amewaasa wadau na washiriki wa mkutano huo kutoa maoni yao yatakayosaidia kupatikana kwa Mkakati huo kwa kuzingatia umuhimu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika maendeleo na ustawi wa jamii na Taifa kwa ujumla.