
Waziri wa Ujenzi Mh. Innocent Bashungwa amesema kuwa Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya miundombinu ya barabara katika Mkoa wa Kigoma, ili kuufanya Mkoa huo kuwa mwanzo wa reli na sio mwisho wa reli katika Sekta ya miundombinu.
Bashungwa ameeleza hayo mbele ya wananchi wa eneo la Kazuramimba, katika ziara ya Makamu wa Rais, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango ya ukaguzi wa utekelezaji wa ujenzi wa barabara ya Malagarasi - Ilunde - Uvinza Mkoani Kigoma.
“Ni maelekezo yako Mheshimiwa Makamu wa Rais, umechoka na ule usemi wa Kigoma mwisho wa reli, badala yake Kigoma iwe mwanzo wa reli na sisi Wizara ya Ujenzi tunaenda kutekeleza hilo kuhakikisha mkoa huu unakuwa Mwanzo wa reli katika sekta ya Miundombinu”. Bashungwa
Aidha. Bashungwa ameeleza kuwa Wizara ya Ujenzi imekamilisha kufanya usanifu wa barabara kuanzia Kibaoni kuelekea Kasulu na hatua iliyopo hivi sasa ni kuendelea kufanya mazungumzo na mfadhili ili nayo iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami.