Benki Kuu ya Tanzania imewataka wananchi kuheshimu fedha ya Tanzania kwa kuwa ni moja ya alama ya taifa na kuonya kwamba kudhihaki na kukejeli noti na sarafu hizo ni kosa la jinai.
Onyo hilo limetolewa leo kufuatia matukio ya hivi karibuni ya baadhi ya wananchi kuzifanyia dhihaka noti za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuzirusha hovyo na wakizikanyaga.
BOT inawakumbusha Wananchi wote kuwa kuharibu noti, sarafu, au kuonyesha dharau ni kosa la jinai kwa mujibu wa kifungu namba 332A cha sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (Penal Code) Sura ya 16 kama ilivyorejewa mwaka 2002.