
Waziri Mkuu Mhe.Kassim Majaliwa, amesema Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) limeahidi kuunga mkono jitihada za Serikali ya Tanzania katika kukuza na kuendeleza sekta ya kilimo.
Amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zina mipango ya kuifanya Tanzania kuwa mzalishaji mkubwa wa chakula ndani ya nchi na ziada kuuza nje ifikapo 2030.
Waziri Mkuu ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Jukwaa la Kimataifa la Chakula Duniani ulioanza Oktoba 16 hadi Oktoba 20, 2023. Waziri Mkuu amehutubia mkutano huo kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.
Waziri Mkuu Majaliwa amesema serikali imeendelea kuimarisha miundombinu mbalimbali ikiwemo ujenzi wa reli ya kisasa, barabara na nishati Vijijini ili kurahisisha shughuli za kilimo.
