Mtu mmoja amefariki dunia na mwingine ambaye ni dereva wa bajaji kujeruhiwa baada ya bajaji aliyokuwa akiiendesha kukigonga Kiberenge, kwenye eneo la makutano ya njia ya reli, eneo la Mazimbu, Manispaa ya Morogoro.
Kamanda wa kikosi cha Zimamoto Mkoa wa Morogoro Kamishna Msaidizi Goodluck Zelote amethibtisha kutokea kwa ajali hiyo majira ya saa saba mchana.
Mashuhuda wa ajali hiyo wamesema baada ya ajali dereva wa Kiberenge alishuka na kusogeza bajaj iliyokuwa kwenye mataruma ya reli na kuendelea na safari huku mwanamke mmoja aliyekuwa abiria wa bajaji akifariki papo hapo na dereva wa bajaji akijeruhiwa vibaya na kukimbizwa hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Morogoro kwa matibabu.
Kamanda wa Polisi Reli, ACP Sebastian Mbuta alipotafutwa kuzungumzia ajali hiyo Kwa njia ya simu, amesema kwa mujibu sheria, dereva wa bajaji ndio mwenye makosa ya kuigonga treni na atachukuliwa hatua kutokana na kosa hilo.