
Ushiriki wa Wadau katika maonesho ya Nane Nane utasaidia kuimarisha muingiliano wa kibiashara kati ya Tanzania na mataifa mbalimbali, ambapo wadau wamehimizwa kutumia fursa hiyo katika kujifunza namna ya kuchangamkia fursa za masoko ya nje.
Akizungumza katika ukumbi wa Kilimo IV, uliopo katika Wizara ya Kilimo jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Dkt. Hussein Omar amesema Wizara imeazimia kuhakikisha Sekta ya kilimo inachangia pato la taifa kupitia biashara na uwekezaji ambapo kwa sasa biashara ya mazao imeendelea kushika hatamu duniani ikihusisha mazao ya chakula na ya kibiashara.
Katika kuhakikisha ushiriki wa pamoja wa matumizi ya teknolojia sahihi za kilimo, wakulima, wafanyabiashara, Taasisi za kifedha pamoja na wadau wa kilimo wizara ya kilimo inaendelea kuwahamasisha kushiriki katika Maonesho ya kilimo ya kimataifa Nane Nane kwa mwaka 2024, ili waweze kuonesha bunifu walizoibua pamoja na kujifunza teknolojia mbalimbali kutoka katika taasisi mbalimbali vikiwemo vyuo vikuu.
Matumizi ya teknolojia bora za kilimo katika kuongeza uzalishaji wenye tija ni miongoni mwa malengo ya Wizara ya Kilimo katika kuhakikisha Taifa linakua kufikia uchumi wa kati wa juu kwa mwaka 2050.