
Kampuni ya Silverlands inayoshughulika na uzalishaji wa vifaranga na chakula cha kuku imeonesha nia ya kuunga mkono Programu ya kielelezo ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya BBT Mifugo ili kuendelea kuwawezesha vijana na akinamama katika sekta ya ufugaji wa kuku lengo likiwa ni kukuza uchumi pamoja na kupunguza mikopo kausha damu kwenye jamii.
Hayo yamefahamika wakati Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega, akizindua mtambo wa kuangua Vifaranga vya kuku katika hafla iliyofanyika Mkoani Arusha.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Kiwanda cha Uzalishaji vifaranga na chakula cha kuku nchini, Silverlands, Dkt Ben Moshi, amesema zaidi ya wafugaji 100,000 wamenufaika na mradi huo wa kuku na wapo tayari kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuwainua vijana na kina mama kupitia programu hiyo ya kielelezo ya BBT.
