Back to top

Rais Magufuli autangaza mji wa Dodoma kuwa jiji kuanzia leo.

26 April 2018
Share

Rais Dkt. JOHN MAGUFULI amewataka watanzania kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya maadhimisho ya  Siku ya Muungano ya mwaka huu isemayo Muungano Wetu ni wa Mfano Duniani Tuuenzi, Tuulinde, Tuimarishe na Kuudumisha kwa Maendeleo ya Taifa Letu.

Rais ametoa changamoto hiyo alipolihutubia taifa kutoka uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma katika maadhimisho ya miaka hamsini na minne ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Amewataka Watanzania waulinde na kuudumisha muungano ambao amesema ni wa kuigwa duniani.

Amiri Jeshi Mkuu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein mara baada ya kuwasili katika jukwa kuu kwa ajili ya maadhimisho ya Sherehe za miaka 54 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar zilizofanyika katika uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma.

Ameyataja baadhi ya mafanikio ya muungano  huo kuwa yamewawezesha Watanzania kudumu katika umoja, amani  na kuheshimiwa na jamii ya kimataifa.

Amewapongeza waasisi wa Muungano Baba wa Taifa Mwalimu JULIUS KAMBARAGE NYERERE na Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati ABEID AMMAN KARUME.

Aidha ameutangaza mji wa Dodoma kuwa jiji  kuanzia leo na kuifanya Tanzania kuwa na majiji sita.

Majiji mengine ni Dar es salaam, Arusha, Mbeya, Mwanza na Tanga.

Maadhimisho hayo yameshereheshwa pamoja na mambo mengine kwa gwaride la heshima lililoandaliwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Watanzania, maonesho ya majeshi ya ulinzi na usalama kuhusu ukakamavu wa kuilinda nchi, halaiki na burudani za ngoma mbalimbali.

Leo ni mapumziko Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dakta REGINALD MENGI pamoja na uongozi wa ITV/Radio One unawatakia  kila la kheri katika maadhimisho ya miaka 54 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.