Salum Shamte amefariki Dunia

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Biashara la nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Taasisi ya Sekta Binafsi nchini Salum Shamte amefariki Dunia asubuhi ya leo katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili alipokuwa amelazwa kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

Marehemu Salum Shamte ameaga dunia leo ikiwa ni wiki moja tangu kuwasili katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya maradhi ambayo yamekuwa yakimkabili.

ITV ilifika nyumbani kwa marehemu Salum Shamte, Boko Jijini Dar es Salaam na kukuta baadhi ya viongozi wa serikali, Taasisi ya Sekta Binafsi pamoja na mamia ya waombolezaji wameungana na familia ya marehemu kusoma dua ya mpendwa wao.

Msemaji wa familia ya marehemu Bwana Hamad Othuman amesema mazishi ya marehemu Salum Shamte yatafanyika kesho Makaburi ya Kisutu.

Marehemu Salum Shamte ameacha wajane watatu na watoto saba.