Back to top

SERIKALI KUANZA KUZITAMBUA SHOROBA ZA WANYAMAPORI NCHINI.

30 June 2023
Share

Kamati ya Kitaifa ya Shoroba za Wanyamapori nchini imefanya ziara ya kuzitambua Shoroba mbalimbali za wanyamapori, ambazo zinakabiliwa na changamoto kubwa kutokana na ongezeko la watu na kuongeza kwa shughuli za kibinadamu katika mapito ya wanyamapori hali inayopelekea madhara makubwa kwa wananchi wanaoishi katika maeneo hayo 

Akizungumza na Waandishi wa habari mkoani Morogoro mara baada ya timu ya wataalam kutembelea ushoroba wa Mwanihana- Magombela unaounganisha Hifadhi ya Taifa Udzungwa, Nyerere na Pori la Akiba la Kilombero, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Lina Kitosi, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Bunge na Siasa, Ofisi ya Waziri Mkuu amesema tembo wamekuwa wakipita kwenye maeneo hayo kwa lengo la kurejea njia zao ambazo ni za awali, hali ambayo imeleta uhaaribifu wa mazao na makazi ya watu pindi wanapopita. 

Kufuatia hatua hiyo, Kitosi amesema Serikali imeanza kuchukua hatua mahsusi ya  kuziongoa  shoroba hizo kwa kuzitambua ili kuwasaidia wananchi kutojihusisha na shughuli za kibinadamu katika mapito hayo ikiwemo kilimo na ujenzi wa makazi.

Ameongeoza kuwa kitendo cha wananchi kuzifahamu na kuzielewa shoroba hizo kutawasaidia   kuepuka kufanya shughuli  kibinadamu katika maeneo hayo na kwa namna hiyo kutapunguza madhara yasababishwayo na tembo .

"Tumetembelea ushoroba huu ambao ni miongoni mwa shoroba 61 za kitaifa ambazo zinapaswa kutambuliwa na wananchi wote , Ili waweze kuzijua na kuzingatia maelekezo yanayotolewa na Serikali katika kuepuka kufanya shughuli zao kwenye maeneo ambayo yametengwa." ameongeza. 

Akielezea hali ya Shoroba nchini,  Dkt. Fortunata Msoffe Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Wanyamapori kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii amesema shoroba nyingi nchini zinakabiliwa na changamoto lukuki ikiwemo ongezeko la shughuli za kibinadamu kwenye maeneo hayo.  

 Amefafanua kuwa kutokana na hali hiyo  Serikali imeamua kuanza kutekeleza  mpango wa kuongoa shoroba hizo kwa kipindi cha  miaka mitano ambapo mpango huo ulizinduliwa na wizara mwaka jana tarehe 17 Septemba 2022.

"Tumeanza na  shoroba za kipaumbele ambazo zilitokana na kazi iliyofanywa na wadau wa maendeleo wakishirikiana na wizara pamoja na wataalam mbalimbali katika kuainisha shoroba Ili kupunguza matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu kwenye makazi ya watu."

 Dkt.Msoffe amesema  katika mpango huo Serikali imeamua  kuanza ni zile shoroba ambazo zipo  hatarini  kutoweka 

"Timu ya Wataalamu leo hii ipo katika shoroba ya  Udzungwa , Hifadhi ya Taifa ya Nyerere kwenda mpaka pori la akiba Kilombero ambayo ni moja kati ya   shoroba 20 ambazo wizara imezipa kipaumbele  

Naye Katibu Tawala wa Kilombero, Abraham Mwaikwila ameishukuru Taasisi ya STEPS chini ya Ufadhili wa  USAID kwa kutoa elimu kwà Wakazi wa Kijiji cha Kanyeja Wilaya ya Kilombero pamoja kuweka fensi ya uzio ambayo imesaidia  kuwazuia tembo ambao wamekuwa  wakiharibu mazao ya Wanakijiji hao pamoja na kuingia kijijini

Ziara hiyo imepangwa kufanyika kuanzia Juni 29 hadi Julai 1, 2023