Back to top

TANESCO Arusha wakamata watu 7 kwa kujiunganishia umeme kinyemela.

06 August 2017
Share

Shirika la umeme mkoa wa Arusha limeendelea na msako wa wezi wa umeme wanaohujumu shirika na kufanikiwa kukamata watuhumiwa saba wilayani Arumeru waliojiunganishia nishati hiyo kinyemela bila kujali madhara yanayoweza kujitokeza ikiwemo uharibifu wa miundombinu ya shirika na hata vifo.

Msako huo umefanyika usiku katika maeneo mbalimbali ya mji mdogo wa Ngaramtoni  na Ilkiding'a ,zoezi ambalo afisa usalama wa TANESCO mkoani humo Dominick Merey anasema ni endelevu na kwamba watuhumiwa wote watafikishwa kwenye vyombo vya sheria .

Akizungumzia athari za miundombinu ya shirika inayosababishwa na uunganishaji huo holela ,mdhibiti wa mapato  wa shirika hilo mhandisi Hassan  Lumuli  anasema  mashine za Transfoma ndizo  zinazoathirika zaidi kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watumiaji tofauti na idadi iliyopangwa.

Baadhi ya wakazi wa Arusha  wanapongeza uwepo wa zoezi hilo ambalo wanashauri  liwe endelevu  kuwabaini wahujumu hao ambao wanasema wamekua chanzo kikubwa cha kupungua kwa umeme.