
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amewakaribisha wawekezaji kutoka nchini Misri kuja kushirikiana na Serikali katika kuwawezesha vijana na wafugaji wengine kufuga kisasa na kunenepesha mifugo kupitia programu ya BBT Mifugo.
Hayo yamefahamika wakati wa ziara ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega na ujumbe kutoka nchini Misri waliyoifanya katika Ranchi ya Kongwa iliyopo Wilayani Kongwa, Jijini Dodoma kwenda kuona namna wanavyoweza kushirikiana katika kuwawezesha vijana na wafugaji wengine kufuga kisasa na kunenepesha mifugo kupitia programu ya BBT Mifugo.
Amesema lengo la Wizara ni kufanya ushirikiano na Wawekezaji hao kuingia mikataba na vijana ya kuwawezesha kuzalisha mifugo bora ambayo itawafanya wawekezaji hao kuwa na uhakika wa kupata nyama bora kwa ajili ya kuuza nchini Misri.

Hivyo, Mhe. Waziri amewashauri wawekezaji hao kuona uwezekano wa kuwawezesha rasilimali fedha vijana kwa njia ya mikataba ili wazalishe mifugo bora ambayo itakuwa chanzo cha uhakika cha wawekezaji hao kupata nyama bora lakini vilevile itawasaidia vijana hao kuwa na uhakika wa ajira kupitia programu hiyo ya BBT mifugo.
Aidha, Mhe. Ulega amesisitiza kuwa kama wawekezaji hao watakuwa tayari kuwezesha vijana kupitia BBT mifugo yeye yuko tayari kuielekeza Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) kushirikiana nao katika kutekeleza programu hiyo katika Ranchi ya Kongwa.
