Back to top

Ulega: "Mchezo wa bao uendelezwe kumuenzi Baba wa Taifa."

11 October 2021
Share

Mbunge wa Jimbo la Mkuranga, ambaye pia ni Naibu Waziri wa mifugo na uvuvi,  Abdallah Ulega ametoa rai kwa jamii kuuendeleza mchezo wa bao  ili kumuenzi Muasisi wake,  Baba wa Taifa ,Hayati, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyefariki dunia 14,oktoba 1999.


Akimkaribisha mgeni rasmi katika fainali ya mchezo wa bao aliyoiandaa ili kumuenzi baba wa Taifa iliyofanyika Wilayani Mkuranga, Mkoani Pwani ,Ulega ameeleza ni muhimu kuendeleza michezo ya jadi ikiwemo mchezo wa bao kwani  ni miongoni mwa michezo ambayo ni kielelezo cha Taifa.


Amesema jambo la kudumisha michezo ya jadi limesisitizwa katika ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), umuhimu wa kurithisha utamaduni kwa watoto na kama  tamaduni zetu hazitaenziwa zitapotea .

"Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan anahimiza michezo, na kuenzi historia ya jadi sana,  Zanzibar hawajawahi kuacha jadi yao hata mwaka mmoja ,ambapo  kila mwaka kuna maonesho ya jadi na mwaka huu yeye mwenyewe alikuwa kinara , kwenye michezo hiyo ya jadi maarufu kama Mwaka kogwa  ili kudumisha masuala ya jadi,"amesisitiza Ulega

Pamoja na hilo ,amewaasa wananchi kuendelea kudumisha amani na upendo  ili kuendelea kumuenzi baba wa Taifa.

Ulega ameahidi kuendeleza mashindano ya mchezo huo kila mwaka ambapo safari hii alitenga milioni moja kwa washindi watatu ambapo mshindi wa Kwanza Vikindu walipatiwa kikombe na sh.500,000, Mwarusembe washindi wa pili 300,000 na Magawa 200,000 ambao ni washindi wa tatu.

"Washindi hawa watatu pia nimewaongeza 50,000 kila timu ili kununua bao mpya,"amefafanua Ulega.

Mcheza bao wa miaka mingi, Selemani Ndugugani amesema michezo hiyo ilianza mwaka 1975 na mwaka 1976 alianza kushiriki michezo hiyo hadi mwaka 1980.

"Michezo hii ya jadi inaonekana kufa lakini tunamshukuru mbunge Ulega kufufua huu mchezo wa bao, unafaida kama soka tu, miaka hiyo mimi mchezo huu ulinifikisha mikoani ya Musoma, Bukoba na Lindi ," amesema Ndugugani

Alimuomba Ulega kuzungumza na wizara ya Utamaduni kuenzi michezo hii na sio soka pekee.

Mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Hadija Nasir amesema mchezo wa bao unaimarisha akili na kuleta furaha .

"Mwanzilishi wa mchezo huu hayati Mwl.Nyerere alidumisha mchezo huu na sisi tunapaswa kuuenzi, " amesema Nasir

Mashindano hayo yalianza ngazi za vijiji na kuunda mashindano ya kata hadi Tarafa na kufuzu kuingia robo fainali .