
Rais Samia Suluhu Hassan, amewataka vijana Watanzania kuilinda amani ya Taifa kwa kulindana wenyewe na kuonesha dunia kuwa yaliyokea Oktoba 29, 2025 hayatatokea tena.
Amesema yaliyotokea Oktoba 29,2025 yalilitia doa Taifa hasa kwa kuwa inaaminika Tanzania ni nchi ya amani hivyo vijana wanamchango mkubwa wa kurejesha amani hiyo.
Rais Samia ameyasema hayo wakati akizungumza na wananchi makundi ya mama lishe, machinga na vijana waliovaa fulana zenye maandishi ya 'Never Again’ waliojitokeza kumsalimia, wakati akianza safari yake ya kutokea mkoani Dodoma kuelekea Dar es Salaam, kwa shughuli za kikazi.
“Vijana wangu nimepokea ujumbe wenu, na niwaombe sana kama kweli mmekusudia ‘Never Again’ kama fulana zenu zinavyosema, naomba mlindane wenyewe kwa wenyewe na msikubali kutiwa maneno ya kuharibu usalama wa nchi yetu na nchi yetu kwa ujumla,” amesema Rais Samia.
Ameeleza kuwa yaliyokea nyuma, yaliwakuta waliohusika na wasiohusika na vijana wengi wakakamatwa, akiwa kama Mama akaamuru waachiwe akiamini wameshajifunza.
"Tanzania ni nchi ya amani hayajawahi kutokea yaliyorokea, sasa tuuoneshe ulimwengu yale yaliyotokea si ya kitanzania na si utanzania ni mambo ya kupandikiza, kwa hiyo sasa tuuoneshe ulimwengu na nawashukuru mmesema hapana ‘Never Again" mesema Rais Samia.
Aidha, amewashukuru vijana hao kwa msimamo huo na kusema kuwa maneno hayo yamempa faraja kubwa.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema maana ya fulana za ‘Never Again’ na zenye rangi ya bendera ya Tanzania ni hawataki tena yaliyotokea Oktoba 29,2025 yatokee.
"Lugha hii ya kwenye fulana ni ya wasomi wa Dodoma wanaokuambia, hawataki tena yaliyotokea tena huko nyuma, wao ni wazalendo, wanaipenda nchi yao, wanaijali na wanaithamini" Amesema Rosemary.
