Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe.Mwita Waitara amewataka watanzania kuondokana na hofu ya kutokamilika kwa mradi mkubwa wa reli ya kisasa ya treni ya mwendo kasi(SGR) kutokana na mabadiliko ya nchi kiutawala kwa sababu lengo la serikali ni kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inakamilika kwa wakati kutokana na umuhimu wake na tayari wameingia mikataba ya makubaliano ambayo ni vigumu kuivunja.
Naibu Waziri Waitara amesema hayo mjini Morogoro baada ya kutembelea na kukagua ujenzi wa kipande cha reli hiyo ya kisasa kutoka Dodoma hadi Dar es salaam na maendeleo ya ujenzi wa stesheni ya SGR ya mkoani Morogoro ambayo ujenzi wake umefikia asilimia 90, na licha ya kubainisha baadhi ya changamoto za kazi hiyo hasa mvua zinazoendelea, akabainisha bado mkandarasi anaendelea vyema na kazi kwa ufanisi mkubwa