Wanafunzi wa Shule ya Msingi Namalombe wilaya ya Nanyumbu mkoa wa Mtwara na Mwalimu mkuu wao Bwanaheri Akili wameiomba serikali kuwajengea madarasa kwani kwasasa wanapata shida kusomea chini ya mkorosho kama darasa, kutokana na shule hiyo kuwa na darasa moja tangu ilipoanzishwa mwaka 2014.
Kwa upande wake Mwalimu mkuu wa shule hiyo amesema wanafunzi wa darasa la saba, darasa la kwanza na darasa awali wanalazimika kusoma chini ya mkorosho huku darasa pili,la tatu,la nne, la tano na darasa la sita wote wakisoma katika jengo la darasa moja lililopo na kufanya kiwango cha kufundisha kuwa kidogo huku wakitumia choo kimoja cha nyasi walimu na wanafunzi.
Hayo yamebainika baada ya ziara ya Naibu waziri wa TAMISEMI David Silinde alipofika shuleni hapo baada ya kupata taarifa kuwepo kwa shule hiyo yenye darasa moja tu na kumuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa halmshauri wilaya ya Nanyumbu mkoa wa Mtwara Hamis Dambaya ndani ya miezi miwili wajenge madarasa manne haraka na kutenga katika bajeti ujenzi wa nyumba za walimu,ofisi na madarasa mengine huku yeye akihaidi atawapelekea madarasa matatu kutoka ofisi ya TAMISEMI.