Back to top

Wananchi Siha walalamikia Jeshi la Polisi kuharibu mazao yao.

28 March 2018
Share

Hekari zaidi  ya 10 za mazao  ya  wakulima  wa  wilaya  ya  Siha mkoani  Kilimanjaro zimeharibiwa  na jeshi  la Polisi  kwa  madai kuwa zimeoteshwa  kwenye  eneo  lililotengwa  kwa  ajili  ya  matumizi  ya  mafunzo hatua ambayo  imelalamikiwa  na  wananchi  na viongozi  wa eneo hilo.
  
Wakizungumzia  suala hilo  wakulima  hao  pamoja na  kukiri  kuwa eneo walilootesha  mazao  hayo lina  mgogoro   wamesema  walishakubaliana  kulitumia kwa  muda  wakati  huu  ambao  halitumiki  lakini   wanashangaa  kuona  mazao  yao  yanaharibiwa.

Mbunge  wa  jimbo  la  Siha Dkt. Godwin  Mollel   amesema  suala hilo lilishafikishwa  kwa  viongozi  wa  ngazi  za  juu  na  lilikuwa   linaendelea  kutafutiwa  ufumbuzi  kwa  njia  ya amani  bila  kuleta  athari   na kwamba  kimsingi  hakukuwa  na  sababu  ya  kuharibu  mazao  ya  wananchi .

Akizungumza  kwa  njia ya  simu  Kamishina  Mwandaizi  Msaidizi  wa  polisi  Ramadhani   Mungi  amesema  eneo  hilo  lipo  kwa  ajili  ya mafunzo  na  kamwe  sio  la  kilimo  na  kwamba kilimo  na  mafunzo  ya  kijeshi  haviwezi  kwenda  sambamba.