Serikali wilayani Chato mkoani Geita imewaonya watu wanajihusisha na uharibifu wa mazingira kwa kuendesha vitendo vya ukataji miti nyakati za usiku kwenye misitu ya asili,hifadhi za taifa, vyanzo vya maji na kuendesha shughuli za kilimo kandokando ya ziwa Victoria kuwa itawachukulia hatua kali za kisheria pamoja na adhabu ya kupanda miti.
Akiongoza taasisi za serkali katika zoezi la upandaji miti katika maeneo yaliyoathirika na ukataji miti mkuu wa wilaya ya Chato injinia Charles Kabeho anasema wameanza operesheni ya kuwabaini watu wanaoharibu mazingira na atakayebainika atapata adhabu ya faini pamoja na kupanda miti mingine katika eneo husika.
Waziri wa nishati ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Chato Dkt.Medard Kalemani amesema kampeni hiyo ya upandaji miti inahusisha zaidi ya miti milioni moja na nusu huku akiwataka wananchi na taasisisi ambazo miti imepandwa kuilinda ili kuhakikisha mazingira yanatunzwa hasa vyanzo vya maji.