
Hali ya sintofahamu imezuka eneo la Tegeta machinjioni baada ya mizoga ya ng'ombe 15 kupelekwa katika machinjio hayo kwa ajili ya kuchinjwa na baadhi ya mizoga hiyo ya ng'ombe kuchinjwa tayari kwa ajili ya kusambazwa katika mabucha ya kuuzia nyama jijini Dare s salaam.
ITV ilifika katika eneo hilo la Tegeta machinjioni na kukuta gari aina ya Isuzu lenye namba za usajili T 486 DHZ lililokuwa na mizoga hiyo ya ng'ombe likiwa limetelekezwa hali iliyolazimu ng'ombe hao kupakiwa katika gari jingine ili wapelekwe kuharibiwa.
Katika eneo hilo maaskari kutoka mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni walilazimika kuimarisha ulinzi ili kuzuia uwezekano wa baadhi ya watu kujichukulia nyama kutoka katika mizoga hiyo na kwenda kuitumia ama kuiuza.
ITV ilifanya jitihada za kuzungumza na Maafisa wa serikali walikuwepo eneo la tukio ambao walikataa kuzungumza na hivyo kumtafuta Meya wa Manispaa ya Kinondoni Benjamin Sitta ambaye alizungumza kwa njia ya simu na kukiri kutokea tukio hili na kuwa watu wawili waliokuwa na mizoga hiyo ya ng'ombe wanatafutwa kwani walikimbia baada ya tukio kubainika.