Back to top

Waziri Mhe.Lukuvi atoa ufafanuzi kuhusu bomoa bomoa aliyoitangaza.

23 October 2017
Share

Waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi Mh. William Lukuvi ametoa ufafanuzi kuhusu  bomoa bomoa aliyoitangaza jumapili akiwa mkoani Rukwa na kusema kuwa bomoabomoa hiyo itawahusu wale wote ambao wamevamia na kujenga nyumba zao katika Viwanja vya watu wengine na siyo watu  ambao tayari wamejenga nyumba zao ila hawakuwa na vibali vya ujenzi.

Mhe. Lukuvi ameyasema hayo alipokuwa akifanya mahojiano maalum na ITV ofisini kwake Dar es Salaam ambapo amesema ,kuna watu wamevamia viwanja vya watu wanyonge na kujenga majumba ya kifahari ili hali wakijua wazi kuwa viwanja hivyo siyo vyao na hivyo amewataka waanze wenyewe kubomoa.

Aidha Mhe waziri amesema siyo ruhusa mtu yeyote kuanzia sasa hivi kujenga nyumba bila ya kibali cha ujenzi na kuongeza kuwa kwa sasa maeneo ambayo awali yalijengwa kiholela serikali haitayabomoa bali itayarasimisha ili hayo makazi yaweze kuwa ya Staha.

Baadhi ya wananchi wamepongeza hatua hiyo ya serikali ya kuwarudishia viwanja watu walioporwa na kusema kuwa kwa miaka mingi Watu wamenyanyasika bila ya kupata msaada kutokana unyonge wao.