Back to top

Waziri Ndumbaro awasili Marekani.

18 January 2022
Share

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro amewasili Jijini  New York, Marekani kwa ajili ya kushiriki mkutano wa  50 wa mwaka  wa Uwindaji wa Kitalii ( Annual Hunting Convention) ulioandaliwa na Jumuiya ya Uwindaji ya Kimataifa.

Mkutano unatarajiwa kuanza 19 Januari, 2022 katika Jiji la Las Vegas, Nevada nchini Marekani umelenga  kuwakutanisha watunga sera na wafanya maamuzi katika ngazi  za juu kutoka nchi  mbalimbali duniani kuweza kujadili masuala ya kisera katika kuendeleza sekta ya uwindaji.

Katika Mkutano huo, Dkt. Ndumbaro anatarajia kunadi fursa za  uwekezaji za uwindaji wa kitalii zilizopo nchini  Tanzania kwa lengo la kuwawezesha Matajiri wakubwa duniani kuchangamkia uwekezaji huo uliopo nchini Tanzania.

Aidha Tanzania ni mshiriki muhimu ikizingatiwa kuwa mojawapo ya nchi zinazoongoza duniani katika uhifadhi wa wanyamapori na uwindaji, hivyo kupitia mkutano  Tanzania itaweza kuongeza uelewa zaidi katika masuala ya kisera na maamuzi katika kuendeleza sekta ya uwindaji wa kitalii nchini.

Katika hatua nyingine,  Dkt. Ndumbaro atapata fursa ya kufanya mazungumzo na Wadau mbalimbali wa masuala ya utalii waliopo nchini ikiwa ni nafasi adimu ya kuwavutia kuja kuwekeza nchini humo.

Katika mkutano huo, Waziri Ndumbaro ameambatana na Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Dkt. Maurus Msuha, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TAWA, Meja Jenerali, Hamis Semfuko, Kaimu Kamishna Uhifadhi wa TAWA, Mabula Misungwi.
 
Wengine ni Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TAWA, Lulu Ng'wanakilala pamoja na Afisa Mhifadhi Mkuu wa Wanyamapori wa kutoka TAWA, Segolin Tarimo

Waziri Ndumbaro pamoja na ujumbe wake wamepokelewa  na Mwenyeji wa  Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mhe. Elsie Kanza.