Wakati ugonjwa wa homa ya Corona ukiendelea kuwa gumzo duniani kadri siku zinavyozidi kwenda hali isiyo ya kawaida imetokea huko nchini India baada ya Madaktari na watoa huduma za afya waliojitolea mstari wa mbele kuokoa maisha ya wanaougua ugonjwa huo kunyanyaswa na kutengwa na wengine kufukuzwa katika makazi yao kwa kuhofiwa kuwa watakuwa wameambukizwa Corona.
Wakati india ikiwa na jumla ya wagonjwa 562 walioripotiwa kuwa na Corona kuna hofu ya hali hiyo kuongeza taharuki na manyanyaso zaidi kwa madaktari na wataalamu wa kutoa huduma ya afya waliojitolea kusaidia kupambana na janga hili huku baadhi ya madaktari wakifukuzwa na wengine kutishiwa kukatiwa umeme.
Wafanyakazi wa hospitali katika mji mkuu wa New Delhi wamesema wamekuwa wakitengwa na kunyanyapaliwa na jamii zao wakihofiwa kuwa na Corona kutokana na kazi yao wanayofanya ya kuwauguza wagonjwa wa corona.