
Mtoto Neema Nassoro (16) mkazi cha Kijiji cha Murwambe Wilaya ya Tarime mkoani Mara, amejeruhiwa kwa kupigwa risasi na watu wanaodaiwa kuwa ni askari wanaolinda mgodi wa North Mara, akiwa katika kibanda cha biashara ya chakula cha mama yake eneo la Murwambe Nyamongo.
Akizungumza hospitalini hapo leo Machi 4, 2024, daktari wa kitengo cha mifupa, Elias Nguti, amesema baada ya kumfanyia uchunguzi wa awali ilibainika binti huyo ana vipande vya chuma kwenye miguu yote miwili.
Neema alifikishwa hospitalini hapo Machi 2, 2024 baada ya kupewa rufaa kutoka Hospitali ya Nyamwaga wilayani Tarime alikopelekwa akitokea katika Kituo cha Afya cha Nyamongo alikopelekwa kwa matibabu baada ya kujeruhiwa.
