
Serikali imetaka kuandaliwa namna bora ya kutoa elimu kwa jamii za mpakani wakati wa zoezi la uimarishaji mpaka wa kimataifa kati ya Tanzania na Rwanda.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Ngara Kanali Mathias Kahabi kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Kagera Hajat Fatma Mwasa wakati wa kikao cha kujadili mpango kazi wa uimarishaji mpaka wa kimataifa kati ya Tanzania na Rwanda.
Kikao hicho kimeanza leo na kinatarajiwa kumalizika tarehe 13 Juni 2025 katika mji wa Ngara mkoani Kagera.
Kanali Kahabi amesema, utoaji elimu kwa jamii zinazoishi mipakani kutajenga uelewa kuwa, zoezi la uimarishaji mpaka wa kimataifa halilengi kutenganisha jamii za mpakani bali ni daraja la kuwajengea mahusiano mazuri wananchi hao.
Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa wilaya ya Ngara, Tanzania na Rwanda zina mambo mengi ya ushirikiano ikiwemo biashara, uwekezaji, uchumi na kidiplomasia hivyo kuwemo kwa kikao hicho katika mji wa Ngara mkoani Kagera ni matokeo ya ushirikiano mzuri kati ya nchi hizo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Hamdouny Mansoor amesema, uimarisaji wa mpaka wa nchi hizo mbili ni utekelezaji wa mpango wa Umoja wa Afrika kuhusu uimarishaji mipaka ya kimataifa kwa nchi za Afrika kufikia mwisho wa mwaka 2027.