
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Dennis Lazaro Londo, amewahakikishia waandishi wa habari nchini kuwa Serikali itaendelea kulinda uhuru wao wa kujieleza pamoja na kuhakikisha wanatimiza majukumu yao kwa usalama na weledi.
Mhe. Londo amezungumza hayo jijini Dodoma katika mafunzo ya waandishi wa habari yaliyowaleta pamoja Wanahabari 100 kutoka maeneo mbalimbali nchini, Mhe. Londo amesema Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaendelea kushirikiana na wadau wa habari katika maeneo yote yanayohusu usalama kwa waandishi wa habari
Aidha, amebainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka msukumo mkubwa katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi, sambamba na kulinda uhuru wa vyombo vya habari.
" Falsafa ya Mhe. Rais kupitia “4R” zinaipa tasnia ya habari nafasi muhimu katika kulinda amani, kuimarisha umoja wa kitaifa na kuendeleza mijadala yenye tija kwa jamii." Amesema Londo
“Ninyi ni mashahidi wa kazi kubwa inayofanywa na Serikali kuhakikisha tasnia ya habari inalindwa kama zilivyo tasnia nyingine muhimu,” Ameongeza Mhe. Londo.
Kadhalika, amesema kuwa mafunzo hayo yatasaidia kuongeza weledi katika kuripoti habari, hususan zinazohusu masuala ya amani na usalama, huku akieleza kuwa waandishi waliohudhuria watakuwa chachu ya maboresho katika tasnia ya habari.
Vilevile, ametumia fursa hiyo kuwashukuru waandishi wa habari kwa ushirikiano mkubwa wanaoutoa kwa Wizara pamoja na vyombo vyake vya usalama
