Back to top

Bomu laua mmoja Kibaha na kujeruhi wawili, polisi waeleza ilivyokuwa.

20 September 2019
Share

Mkazi wa Kibaha Msangani mkoani Pwani, Mbaraka Koromera mwenye umri wa miaka 37 amefariki na wengine wawili kujeruhiwa kutokana na mlipuko mkubwa wa kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu wakati akichambua vyuma chakavu kwenye nyumba isiyoisha maarufu kama Pagale.
 
Kamanda wa polisi mkoa wa Pwani ACP Wankyo Nyigesa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake amethibitisha kutokea kwa tukio hilo mapema majira ya saa nne asubuhi ambapo saa tano mbaraka alikutwa na umauti huo na majeruhi wawili kukimbizwa katika hospitali teule ya Tumbi Kibaha mkoani Pwani.

Aidha Kamanda Wankyo amewataja waliojeruhiwa katika tukio hilo kuwa ni Fatuma Likupila maarufu kama Mama Tabu ambaye alipata majeraha kichwani na hali yake ni mbaya kwakuwa alikuwa anatokwa na damu masikioni huku Shomari Athumani akijeeuhiwa mwili mzima baada ya kuchanwa na vitu vyenye ncha kali vilivyomsababishia jeraha kubwa mapajani na sehemu za tumboni. 
 
Kufuatia kutokea kwa tukio hilo timu ya wataalamu kutoka jeshi la polisi kwa kushirikiana na jeshi la wananchi wa Tanzania wanaendelea na uchunghzi ili kubaini mlipuko huo kama ni bomu ama la ama ni aina gani ya bomu huku likitoa rai kwa wananchi kutoa tarifa wanapoona vitu vyenye mashaka kwenye maeneo yao.