Kufuatia malalamiko ya ongezeko la bei kwa nauli za mabasi yaendayo mikoani baraza la ushauri la watumiaji wa huduma za usafiri wa nchi kavu na majini SUMATRA limesema hakuna ongezeko lolote la nauli ambapo wamesema watahakikisha watoa huduma wasiofata taratibu wanachukuliwa hatua.
Akizungumza na waandishi wa habari katibu mtendaji wa baraza hilo Dakta Oscar Kikoyo amesema yeyote atakayebainika atachukuliwa hatua na amewataka abiria kuhakikisha wanasafiri kwa tiketi yenye majina yao na iliyoandikwa kiwango sahihi cha nauli wanayolipa.
Aidha dakta Kikoyo ameutaka umoja wa wamiliki wa mabasi TABOA kuhakikisha madereva wao wanazingatia kanuni za usafirishaji za mwaka 2017 ambavyo vinakataza maubiri ya dini ama siasa pamoja na kuzingatia maadili ya video ambazo zinaonyehswa katika mabasi.
Imekuwa kawaida kwa mabasi yaendayo mikoani kupandisha nauli kila ifikapo mwishoni mwa mwaka jambo ambalo limekuwa likilalamikiwa na abiria ambapo sambamba na hilo SUMATRA imewataka TABOA kudhibiti madereva wao ambao huendesha kwa kasi kusudi wageuze siku hiyo hiyo ili kutengeza fedha.
