
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amewaonya baadhi ya watu au makundi ya watu wenye nia isiyo njema kwa zoezi la Sensa ambao wamekuwa wakitoa matangazo ya ajira za Sensa kwa nia ya kuwatapeli wananchi wanaohitaji kushiriki katika zoezi hilo.
Waziri Simbachawene ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuanza kwa mchakato wa Ajira za Makarani na Wasimamizi wa Sensa ya Watu na Makazi itakayofanyika Agosti 23, 2022 Nchi nzima.
Pia Mhe.Simbachawene amesema kwamba mchakato wa ajira za makarani na wasimamizi kuanzia Mei 05 hadi Mei 19,2022 ambao utahusisha ngazi zote za kiutawala kuhakikisha wanapatikana makarani na wasimamizi wenye sifa stahiki.
“Kumekuwepo na watu au makundi ya watu wenye nia isiyo njema kwa zoezi la sensa ambao wamekuwa wakijaribu kutoa matangazo ya ajira za Sensa kwa nia ya kuwatapeli wananchi wanaohitaji kushiriki katika zoezi hili na pengine kwa nia ya kuvuruga mchakato mzima,”amesema Mhe. Simbachawene.
Vilevile Mhe.Simbachawene aliwahimiza watanzania wote wenye sifa ambao wangependa kuomba nafasi za ajira hizo kufuata utaratibu uliowekwa kwa ukamilifu ili kuomba nafasi hizo.
"Kazi za kufanya pamoja na sifa za mwombaji zimebainishwa katika Tangazo la Ajira za Muda za Makarani na Wasimamizi wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022.Hakutakuwa na maombi yatakayofanyiwa kazi zaidi ya yale yatakayofuata utaratibu uliowekwa mtandaoni"Alifafanua Mhe.Simbachawene.
Kuhusu namna ya kufanya maombi hayo alibainisha kwamba waombaji watatakiwa kutuma maombi yao kupitia mtandao (Online) ambao hautahusisha malipo yoyote kwa mwombaji wa ajira.
