Back to top

RAIS DKT.SAMIA ATAKA WANAWAKE KUSHIRIKISHWA KULETA MAENDELEO

03 December 2022
Share

Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali itaendelea kuwashirikisha wanawake kwa kuhakikisha inatanua mtandao wa wanawake katika sekta mbalimbali.

Rais Samia amesema hayo leo katika Kongamano la Nne la Wanawake Vijana wa Mtandao wa Viongozi Wanawake Barani Afrika (African Women Leaders Network - AWLN) lililofanyika Zanzibar.

Aidha, Rais Samia amesema lengo la kuwashirikisha wanawake ni kuweza kufikia ajenda ya 2030 ya Maendeleo Endelevu, Ajenda ya Umoja wa Afrika ya 2063 pamoja na Dira ya Maendeleo ya Tanzania ya 2025.

Rais Samia pia amesema maendeleo ya wanawake yamekuwa yakiathiriwa na changamoto mbalimbali kama kutokupata rasilimali, kutengwa, kutokupata haki zao na kutokupewa nafasi katika kufanya maamuzi.

Vile vile, Rais Samia amesema takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2021 idadi ya wanawake walioajiriwa ilishuka ambapo wanawake milioni 45 duniani waliondoka katika ajira mwaka 2021 na hivyo kuwafanya kuwa maskini zaidi.

Hata hivyo, Rais Samia amesema Tanzania inafanya jitihada ya kuwashirikisha wanawake katika vyombo vya kufanya maamuzi akitolea mfano kuongezeka kwa idadi ya Wabunge kutoka 21.5% mwaka 2005 hadi 37% mwaka 2022 na Mawaziri 9 katika Baraza la Mawaziri.

AWLN ni mtandao ambao unataka kuhakiksha kuwa wanawake wana sauti katika nyanja zote za maisha kwa kutekeleza Malengo Endelevu ya Umoja wa Mataifa na kufikia Malengo ya AU ya kufikia Afrika tunayoitaka.