
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt.Pindi Chana, ameziagiza taasisi za uhifadhi, zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii, ziweke alama za kudumu zinazoonekana kwenye mipaka ya hifadhi, kwa kuzingatia maamuzi yaliyoelekezwa na Baraza la Mawaziri, ili kuepusha migogoro ya ardhi kati ya wananchi na maeneo yaliyohifadhiwa kisheria.
Dk.Chana ameyasema hayo Jijini Dodoma, wakati wa kikao kazi cha kujenga uelewa wa pamoja kuhusu Uhifadhi endelevu wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha na Bonde la mto Usangu, kilichohusisha timu za wataalam wa Wizara hiyo kutoka Idara ya Wanyamapori, Sera na Mipango, Sheria pamoja na Wataalam kutoka Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Taasisi ya WanyamaporTanzania (TAWA) na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).
Balozi Dkt. Chana ameeleza kuwa, Serikali inaendelea na jitihada za kufanya maboresho katika sekta ya Maliasili na Utalii hususani kwenye uhifadhi endelevu hivyo juhudi hizo zinapaswa kuungwa mkono.
