
Makandarasi wazawa wametakiwa kuzisimamia kampuni zao kwa ufasaha kwa kufuata sheria za manunuzi ya umma, ulipaji wa kodi kwa wakati na kufanya kazi kwa weledi kwa kutumia wataalamu stahiki katika sekta mbalimbali ili kukwepa changamoto katika maeneo yao ya kazi.
Akizungumza katika mafunzo ya siku 3 yenye lengo la kuwajengea uwezo Makandarasi wazawa kibiashara, jijini Dar es Salaam, Msajili wa Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB), Mhe.Rhoben Nkori, amesema kuwa lengo moja wapo ni kutoa elimu kwa makandarasi kuhusiana na mfumo mpya wa manunuzi kwa Umma (Nest) na hii inatokana na kuwa na mabadiliko makubwa ya sheria ya manunuzi ya umma na tayari sheria ipo katika hatua za mwisho kabla haijawa sheria kamili.

"Biashara ya Ukandarasi ni kubwa na kuanzia mwanzo ni unaingia kwenye mifumo inayostahili na unadhibitiwa. Mifumo ya CRB ni miongoni iliyounganishwa na Nest na mkandarasi hatoweza kufoji wala kudanganya chochote pale atakapokua anaingiza taarifa zake"Alisema Msajili.
Mhe.Nkori amesisitiza kuwa makandarasi wabadilishe mtazamo wao na kuwa wafanyabiashara wa kweli na halali bila kukwepa kulipa kodi, kufoji nyaraka na kufanya kazi kwa weledi na kwa kuzingatia sheria za nchi.
Aidha Mhe. Nkori, amesema makampuni mengine hutumika kufanya kazi kwa majina ya wamiliki wengine yanayopelekea mvutano pindi kazi inapoenda kukaguliwa na TRA kupitia Bodi ya Usajili wa Makandarasi(CRB) hivyo amewataka wamiliki wa makampuni kusimamia vyema makampuni yao ili kuepuka changamoto hizo.
Mhe.Nkori amesisitiza kuwa ili kuendelea kujenga taswira nzuri kwa makandarasi nchini, Bodi itaendelea kuwachukulia hatua kisheria makandarasi wote wanaokiuka maadili yao ya kazi.
