Back to top

REGROW YAZIDI KUWA NEEMA KWA WANA TUNGAMALENGA

03 November 2023
Share

Dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan ya kuwainua wananchi kiuchumi kupitia Mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Nyanda za juu Kusini (REGROW) inapaswa kuungwa mkono na wanavikundi vyote vilivyowezeshwa na Mradi huo kwa kuhakikisha fedha hizo zinatumika kwa malengo sahihi.

Wito huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Kamishna Benedict Wakulyamba, Kijiji cha Tungamalenga Mkoani Iringa,  alipokuwa akikagua utekelezaji wa miradi ya wanavikundi ilivyopatiwa fedha na Mradi wa REGROW kwa lengo la kujikwamua kiuchumi.

Mzee wa Boma la jamii ya Kimasai Kijiji cha Tungamalenga,  Matambile Lemkamilo, amepongeza jitihada za Serikali kupitia mradi wa REGROW kwani jamii yake kwa sasa licha ya maendeleo zaidi ya kiuchumi pia imekuwa rafiki zaidi wa Hifadhi ya Taifa Ruaha hali inayopelekea kushiriki vyema katika ulinzi wa Hifadhi hiyo.

Msimamizi wa Kipengele cha pili cha Mradi wa REGROW Bi. Hobokela Mwamjengwa amebainisha kuwa zaidi ya Bilioni  1.8 zimetolewa  katika vijiji 16 vinavyopakana na hifadhi ya Taifa Ruaha, fedha hizo zimetumika kutoa fedha mbegu kwenye vikundi vya COCOBA 53, miradi ya kuzalisha kipato kwa vikundi 53.

Ameongeza kuwa kupitia fedha hizo, REGROW imetoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi 120,kutoa mafunzo kwa askari wanyamapori wa vijiji 121 na hadi sasa wananchi zaidi ya 3,800 wamenufaika na utekelezaji wa mradi huo kwenye vijiji hivyo 16.