
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega ameelekeza kuondolewa katika nafasi yake Kaimu Mkurugenzi wa Uvuvi, Bw. Stephen Lukanga baada ya kushindwa kupanga na kutekeleza mikakati thabiti ya kukomesha uvuvi haramu nchini.
Waziri Ulega ametoa maamuzi hayo wakati akikabidhi boti (11) yenye thamani ya Shilingi ya Bilioni 1. 85 yaliyotolewa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) kwa mkopo kwa wavuvi wa Mkoa wa Dar es Salaam leo.
Waziri Ulega amefika maamuzi hayo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wadau wa Uvuvi Mkoani Dar es Salaam ya kukithiri kwa vitendo vya Uvuvi haramu katika ukanda Pwani hususani Dar es Salaam.
Oktoba 4, 2023 akiwa mkoani Mwanza katika Soko la Lumumba, Waziri Ulega alimtaka Kaimu Mkurugenzi huyo kuwa ndani ya Mwezi mmoja kuhakikisha anapanga na kutekeleza mikakati thabiti ya kukomesha uvuvi haramu nchini ambao kwa muda umekuwa ni kikwazo kwa maendeleo ya sekta ya uvuvi.