Back to top

DMO NA MFAWIDHI MBOZI WASIMAMISHWA KAZI

16 February 2023
Share

Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel, ameagiza Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mbozi na Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya hiyo wasimamishwe kazi , baada ya viongozi hao kushindwa kutoa ufafanuzi juu ya matumizi ya fedha, kiasi cha shilingi milioni 178, baada ya makusanyo ya jumla ya shilingi milioni 498,297,598.
.
Dkt.Mollel ameyasema hayo wakati akikagua utoaji huduma na uboreshaji wa miundombinu ya Afya kwenye Wilaya hiyo, ikiwa ni kutekeleza maelekezo ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa.
.
Amesema, Serikali ya Rais Samia umekuwa ikifanya maboresho makubwa katika huduma za afya, ikiwemo kuleta fedha za vifaa tiba, fedha za manunuzi ya dawa na kuboresha miundombinu, lakini wapo baadhi ya viongozi wanashindwa kuendana na kasi ya Rais Samia na wengine wanafanya matumizi mabovu ya pesa za wananchi hii haiwezekani.
.
Sambamba na hilo, Dkt. Mollel amesema, uamuzi wa kuelekeza mamlaka kuwasimamisha viongozi hao, ni kutokana na kushindwa kutoa ufafanuzi juu ya matumizi ya kiasi cha shilingi milioni 178 baada ya makusanyo ya jumla ya shilingi milioni 498,297,598.
.
Aidha, Dkt. Mollel ametoa wito kwa Watumishi wote hususan waliopo katika Sekta ya Afya kufanya kazi kwa juhudi na kufuata miongozo na maadili ya taaluma zao pindi wanapofanya kazi ili kuondokana na vitendo viovu ikiwemo ubadgilifu wa fedha za umma.