Back to top

KOCHA MWALAMI, KAMBI WAFIKISHWA MAHAKAMANI

21 November 2022
Share

Aliyekuwa Kocha wa makipa wa Klabu ya Soka ya Simba ya jijini Dar es Salaam, Mwalami Sultan na mmiliki wa Kituo cha Soka cha Kambiasso Sports Academy kilichopo Tuangoma wilayani Kigamboni, Kambi Seif na wenzao wanne wamefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka mawili ya kusafirisha kilo 34.89 za dawa za kulevya.
.
Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo na wakili wa Serikali Mwandamizi, Grace Mwanga imewataja washtakiwa wengine kuwa ni, Maulid Mzungu, Said Matwiko, John Andrew John na Saraha Eliud.
.
Imedaiwa mbele ya Hakimu mkazi Mkuu Mary Mrio kuwa, Oktoba 27, 2022 huko katika eneo la Kivule lililopo ndani ya Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam,  washtakiwa walikutwa wakisafirisha kilo 27.10 za dawa za kulevya aina ya Herione.
.
Katika shtaka la pili imedaiwa Novemba 4, 2022 huko Kamegele katika Wilaya ya Mkuranga Mkoani Pwani washtakiwa walikutwa wakisafirisha kilo 7.79 za dawa za kulevya aina ya Heroine. 
.
Hata hivyo, baada ya kusomewa mashtaka hayo, washtakiwa hawakuruhusiwa kujibu chochote mahakamani hapo kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi.
.
Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika na kesi imeahirishwa hadi Desemba 5, 2022.