
“Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mkuu wa Mkoa Mstaafu Ndg. Abbas Kandoro, nawapa pole wana familia, ndugu, jamaa na marafiki wote walioguswa na msiba huu, pamoja na wananchi wa mikoa ya Tabora, Arusha, Dar es Salaam, Mwanza na Mbeya ambako aliwahi kuwa Mkuu wa Mkoa.
Tumempoteza mtu muhimu ambaye mchango wake katika utumishi kwa umma katika nyadhifa mbalimbali zikiwemo Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi wa halmashauri hautasahaulika.
Ndg. Abbas Kandoro alikuwa kiongozi shupavu, aliyejiamini na kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria na taratibu, aliwapenda watu aliowaongoza na alidhirisha uzalendo wa kweli.
Nimesikitishwa sana na kifo chake, nawaombea wafiwa wote wawe na moyo wa subira, uvumilivu na ustahilivu katika kipindi hiki cha majonzi na pia namuombea Marehemu Abbas Kandoro apumzike mahali pema peponi, Amina”
Ni sehemu ya salamu za rambirambi alizozitoa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kufuatia kifo cha Mkuu wa Mkoa Mstaafu Ndg. Abbas Kandoro kilichotokea jana jioni tarehe 27 Aprili, 2018 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili Jijini Dar es Salaam.
Mhe. Rais Magufuli amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bi. Amina Masenza kufikisha salamu hizo kwa familia ya Marehemu, ndugu, jamaa, marafiki na wote walioguswa na msiba huo.