Shirika la Mpango wa Chakula Duniani, limesitisha kwa muda usambazaji wa misaada ya kibinadamu huko Beni, nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kutokana na mashambulio yanayoendelea kwenye maeneo yenye mlipuko wa ugonjwa wa ebola.
Msemaji wa shirika hilo HERVÉ VERHOOSEL amewaambia waandishi wa habari mjini Geneva, Uswisi kuwa shirika limechukua hatua hiyo kwa sababu wafanyakazi na wadau wake hawana uhakika wa usalama wao na kwamba kuna ugumu kufikia maeneo ambako misaada inapaswa kupelekwa.
Amesema kutokana na hali hiyo shirika linahofu kuwa hali ya kibinadamu itakuwa mbaya kwa sababu watu wengi watahitaji misaada ya hali na mali.
Ghasia zimekuwa zikiongezeka katika mji wa Beni tangu kuanza kwa operesheni inayoongozwa na serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo dhidi ya kikundi cha waasi cha ADF iliyoanza tarehe 30 Oktoba mwaka huu.