Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe.Mussa Azzan Zungu amesema kwamba mifuko inayoingizwa kwa njia za panya kutoka nchi jirani ambayo hailipiwi kodi, inaathiri mazingira na soko la uzalishaji wa mifuko yenye viwango na ubora kutoka Tanzania.
Akizungumza kwenye kipindi cha Kumepambazuka kinachoruka Radio One Mhe.Zungu amesema elimu wameshatoa kwa wananchi ya namna ya kutambua mifuko isiyo na ubora hivyo kwa atakayekutwa akitumia mifuko hiyo adhabu yake atatozwa shilingi elfu 30 mpaka laki mbili na kifungo cha siku 7 huku mtengenezaji na msambazaji akitozwa milioni 20.
Mhe.Zungu amesema mifuko hiyo isiyo na viwango imeanza kurudi nchini kutokana na kuwa na vishawishi vya pesa ambapo kontena moja la mifuko mbadala inaweza kuuzwa mpaka milioni 150.
Amewataka wenye viti wa Serikali za Mitaa na wananchi kutoa taarifa pale wanapobaini kuwepo kwa viwanda bubu vidogo vidogo vinavyotengeneza mifuko hiyo.